Taasisi ya Lady Fatemah Trust yenye makao yake nchini Uingereza kwa kushirikiana na taasisi ya Bilal Muslim Mision of Tanzania (BMMT) wamekabidhi mradi wa ukarabati wa vyoo katika shule ya msingi Mtendeni iliyopo jijini Dar es salaam.
Hafla ya makabidhiano ya mradi huo imefanyika tarehe mosi Septemba, 2022 katika viwanja vya shule hiyo na ilipata heshima ya kushudiwa na Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Ilala Mheshimiwa Mussa Azan Zungu.
Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na uongozi wa BMMT, ukiongozwa na Mwenyekiti – Husein Karim, Afisa Mtendaji Mkuu – Hafidh Mansour na Mkuu wa Tabligh Taifa – Sheikh Msabaha Mapinda huku Lady Fatema Trust ikiwakilishwa.
Wengine ni viongozi wa kisiasa na serikali, waalimu, wanaafunzi na wadau wengine.
Akizungumza kwa niaba ya Lady Fatemah Trust, Afisa Mtendaji Mkuu wa BMMT Hafidh Mansour amesema, taasisi zote mbili zinaamini katika elimu na kwamba mazingira bora yanamchango mkubwa katika maendeleo ya sekta ya elimu.
Shule ya msingi Mtendeni ni miongoni mwa shule kongwe nchini Tanzania, ilianzishwa mnamo mwaka 1937 na ilikuwa chini ya uangalizu wa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mnamo mwaka 1967.
Mgeni wa heshima, Mh. Zungu amezipongeza taasisi za Lady Fatemah Trust na washirika wao BMMT kwa mchango wao kwenye sekta ya elimu nchini lakini pia alitumia hafla hiyo kutoa wito kwa taasisi na watu wengine kushiriki kwenye harakati za kuleta maendeleo nchini akisisitiza kuwa, suala lamaendeleo sio jukumu la serikali pekee.
Ukarabati uliofanyika umelihusu jengo lote la vyoo vya shule hiyo, ikiwa pamoja na kuweka mfumo mpya wa maji safi na taka, uwekaji marumaru kwenye sakafu na ukutani, ujenzi wa vizimba vya kunawa pamoja na kupaka rangi jengo pamoja na paa ambapo kwa ujumla, takriban shilingi milioni 25 za kitanzania zilitumika.
Khadija Jailani ni mwanafunzi wa darasa la saba katika shule ya msingi mtendeni, wakati akitoa risala mbele ya mgeni rasmi alitoa shukrani zake za dhati kwa niaba ya wanafunzi wenzake kwa taasisi za Lady Fatemah Trust pamoja na BMMT kwa jitihada zao za kuboresha mazingira ya shule hali ambayo itasaidia kuepuka magonjwa ya mripuko kama vile kipindupindu, kuhara na homa za matumbo na hiyo kuweka mazingira bora kwa ajili ya kujifunza.
Shule ya msingi Mtendeni ina jumla ya wanafunzi 1303, kati yao wasichana ni 654 na wavulana 649.
Bofya hapa kutazama video – tukio la kukabidhi mradi (English)