Taasisi ya Bilal Muslim Mission of Tanzania (BMMT) imeshiriki kikamilifu kwenye maonesho ya Husein Day mwaka 2022 yaliyofanyika kwa muda wa siku tatu mfululizo (Aug 25-27) katika viwanja vya Mnazi mmoja jijini Dar es salaam.
Pamoja na mambo mengine, BMMT ilipata fursa ya kuonesha kazi mbalimbali zinazofanywa na taasisi hii katika kuihudumia jamii ya Watanzania kote nchini.
Wageni mbalimbali walishiriki kwenye maoenesho hayo kwa nyakati tofauti wakiwemo viongozi wa dini kama vile Sheikh mkuu na Mufti wa Tanzania – Dkt. Abubakar bin Zubeir, Sheikh mkuu wa Dar es salaam – Alhad Mussa Salum, Sheikh Mkuu wa T.I.C – Sheikh Hemed Jalala, Mkuu wa Tabligh BMMT taifa – Sheikh Msabaha Shabani Mapinda, Naibu spika wa bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Ilala – Mh. Mussa Azan Zungu, Meya wa jiji la Dar es salaam- Mh. Omar Kumbilamoto, viongozi wa taasisi mbalimbali ikiwa pamoja an viongozi wa ngazi ya juu wa BMMT na wananchi wengine.
Maonesho hayo yaliandaliwa na Jumuiya ya Kiislamu ya Khoja Shia Ithna-ashari Jamat kwa ushirikiano na taasisi nyingine za madhehebu ya Shia Ithna-ashari.
Katika kipindi chote cha siku tatu mambo kadhaa yalifanyika ikiwa pamoja na kutolewa kwa hotuba mbalimbali zenye mafunzo ya Imam Husein (a).
Zaidi ya maonesho ya kazi mbalimbali zinazofanywa na taasisi zilizoandaa kambi hiyo, pia kulikuwa na huduma za upimaji wa afya kwa maradhi yasiyoambukiza kama vile kisukari, shinikizo la damu, na huduma ya kupima macho na vyote vilitolewa bure. Sambamba na hayo kambi hii iliendesha zoezi la uchangiaji damu na kiasi cha chupa zaidi ya elifu moja zilipatikana.
RIPOTI – BILAL TANZANIA KATIKA KUMBUKUMBU YA KIFO CHA IMAM HUSEIN (A)- MUHARRAM, 1444 HIJIRIA